Monday, August 19, 2013

Bagamoyo yaanza kujifadhili vita dhidi ya UKIMWI,VVU

Bi Albina, CHAC wa Bagamoyo akitoa taarifa ya hali ya UKIMWI wilayani humo kwa wajumbe wa TACAIDS waliotembelea Mkoa wa Pwani juzi
Kamishna wa TACAIDS Dk.Rose Mwaipopo akitoa majumuisho ya ziara ya tume Wilayani Bagamoyo. Katikati ni Kaimu Mkurugenzi wa Bagamoyo Bw. Erasto Mfugale na kulia kabisa ni RCT wa Pwani Dk.Ameir
Wana-kikundi cha UWAMABA--kikundi cha watu waishio na VVU wilayani Bagamoyo na moja ya vikundi vilivyofanikiwa katika kampeni dhidi ya UKIMWI--wakiwa katika picha ya pamoja na ujumbe wa TACAIDS
HUKU ufadhili katika masuala ya huduma za UKIMWI nchini ukielekea ukingoni, Halmashauri ya Bagamoyo sasa imetangaza kutenga shilingi milioni 25 kuanzia msimu wa 2013-2014 kwa ajili ya kuendeleza mapambano dhidi ya UKIMWI na virusi vya UKIMWI (VVU) wilayani hapo.

Hayo yamebainishwa juzi na Mratibu wa UKIMWI-Pwani (CHAC) Bi Albina Mtumbuka alipokutana na ujumbe wa tume ya kudhibiti UKIMWI nchini (TACAIDS) uliotembelea ofisini kwake katika ziara iliyolenga kujua hali ya UKIMWI na vichocheo vyake katika mkoa wa PWANI.

Ujumbe wa TACAIDS uliongozwa na Kamshna wa Tume hiyo Dr Rose Mwaipopo.

“Tumeamua kutenga kiasi hicho (shilling mil.25) kuanzia mwaka huu wa fedha ili kuepusha balaa linaloweza kutokea kutokana na kujitoa kwa wafadhili ambao wamekuwa wakitusaidia tangu tulipoanza vita dhidi ya UKIMWI,:” akasema Bi Mtumbuka

Bagamoyo ni miongoni mwa wilaya zilizo athirika na maambukizi ya VVU nchini.  Kwa mujibu wa matokeo muhimu ya utafiti wa viashiria vya VVU-UKIMWI na Malaria (THMIS 2011-2012), maambukizi ya VVU yalikuwa yamefikia asilimia 6.9

Kwa mujibu wa Bi Mtumbuka, endapo wilaya haitachukua hatua madhubuti, ni wazi kuwa mafanikio yaliyokuwa yamefikiwa katika kutoa huduma mbalimbali za vita dhidi ya UKIMWI yatakuwa hatarini.

“Hatuna jinsi, kujitoa kwa wafadhili wetu kuwe changamoto kwetu ya kujua namna ya kuendeleza mapambano haya, “ akaongeza Bi Mtumbuka.

Taarifa zilizomfikia mwandishi wetu ni kwamba wafadhili ambao wamekuwa wakitoa pesa kwa ajili ya mfuko wa mwitikio wa UKIMWI katika wilaya zote nchini kupitia TACAIDS (NMSF) wametangaza kusitisha ufadhili wao kuanzia mwaka kesho (2014).

Baadhi ya wafadhili hao ni kutoka mataifa ya Canada (CIDA) na Denmark (DANIDA). “Hali itakuwa ngumu katika halmshauri zetu mara jamaa watakapojiondoa rasmi mwaka kesho—hatutakuwa na jinsi zaidi ya kila wilaya kuanza kujichangisha ili mafaniko tuliyoyafikia dhidi ya UKIMWI yasiwe kazi bure, kilisema chanzo chetu.

Kama hakutakuwa na hatua madhubuti za kila wilaya kutafuta vyanzo vingine vya fedha za kukabiliana na UKIMWI, huduma kama vile matibabu kwa wanaoishi na VVU (ARVs), huduma za UKIMWI majumbani, upimaji wa VVU na huduma kwa watoto yatima vyote vitakuwa katika hatari ya kusambaratika, akabainisha Bi Mtumbuka wakati wa majumuisho yake

Katika miezi ya hivi karibuni, TACAIDS na wadau wengine wake wamekua wakihaha kuharakisha uundwaji wa mfuko wa UKIMWI nchini (AIDS Trust Fund). Tume inaamini kuwe uundwaji wa mfuko huo utasitisha utegemezi wa wafadhili katika masuala ya UKIMWI.

“Ni kweli kabisa, kama mfuko huo utapitishwe na bunge, ni dhahiri tutakuwa katika mazingira mazuri kuendeleza kampeni zetu. Hatutakuwa na haja ya kubabaika kama ilivyo sasa,:” alisema Dk. Hafidhy Ameir, Mratibu wa TACAIDS mkoani Pwani

Kuhusu hali ya maambukizi ya VVU Bagamoyo, takwimu za watu waliojitokeza kupima kwa hiari zinaonesha kuwa kuanzia Januari hadi Desemba 2012 jumla ya watu 19,126 walishauriwa na kupima VVU. Kati ya hao wanaume ni 5,804 na wanawake ni 13,322.

Ukiwa ni mmoja wa miji mikongwe na ya kitalii nchini, Bagamoyo imeathirika zaidi na maambukizi ya VVU kutokana na kuwa na watu wengi wenye tabia na kutoka maeneo tofauti hali inayopelekea kuwa na miingiliano holela ya wa ki-ngono zembe.

0 comments:

Post a Comment