Thursday, June 26, 2014

Kampeni ya Linda Goli Lako yaanza Tanzania

Asasi ya Vijana wa Umoja wa Mataifa Tanzania (YUNA) kwa kushirikiana na Umoja wa Mataifa hivi karibuni wametangaza kuanza kwa kampeni ya “Linda Goli Lako” nchini Tanzania.
“Linda Goli lako” ni mpango wa kimataifa unaosimamiwa na Mradi wa Pamoja wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa kushughulikia UKIMWI (UNAIDS) wa kuongeza uhamasishaji kuhusu kujikinga na maambukizi ya virusi vya ukimwi (VVU) duniani kote kwa kupitia michezo na sekta ya muziki.
Vijana kutoka mashirika ya UN walioshiriki katika kampeni hiyo. (kushoto-kulia) ni: Dk Yeronimo Mlawa (UNAIDS), Usiah Nkhoma (UNIC), Sawiche Wamunza (UNFPA) na kiongozi wa YUNA Tanzania (jina halikupatikana)
Kampeni ina lengo la kuongeza ufahamu wa VVU na kuhamasisha vijana kujikita katika Kuzuia Maambukizi ya VVU (Matumizi ya kondomu, upimaji virusi vya Ukimwi kwa hiari, na kupunguza
idadi ya wapenzi).
Nchini Tanzania, kampeni hii inajulikana kwa Kiswahili kama ‘’Linda Goli Lako, kavukavu nomaa’’ kampeni hii ilianza kabla ya kombe la dunia 2014 na itaendelea baada ya kumalizika kwa fainali za kombe hilo.
Lengo ni kuwafikia vijana mbalimbali kwa ujumbe tofauti wa VVU na Mpango Kabambe wa Afya ya Uzazi (SRH) kupitia michezo na vyombo vya habari.
Uhamasishaji wa kampeni hiyo hususan suala la mabadiliko ya tabia zitahusisha, pamoja na mambo mengine, matumizi ya mitandao ya kijamii, michezo hususan mchezo wa mpira wa miguu kama fursa ya kutoa ujumbe na kukuza uelewa wa vijana kuhusu masuala ya afya ya uzazi. Watoa huduma za afya ya uzazi pia watahamasishwa kupitia washirika mbalimbali ili kutoa huduma wakati wowote ambapo vijana watakusanyika kwa ajili ya shughuli za michezo.
Katika wiki ya kampeni kulikuwa na mfululizo wa shughuli za kampeni katika kuhitimisha uzinduzi rasmi wa kampeni ikiwamo vipindi vya redio na televisheni.
YUNA kwa kushirikiana na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo Cha Diplomasia (CFR) na Chuo Cha Biashara (CBE) walifanya mashindano ya siku mbili ya kandanda Kabla ya Kombe

la Dunia katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Hosteli za Mabibo siku ya Jumamosi Juni 7 na Jumapili 8 Juni, 2014 kwa vyuo vikuu vilivyopo Dar es Salaam.
Mgeni rasimi katika uzinduzi huo alikuwa Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Linus Mgaya. Ujumbe wa kampeni kwa vijana ulizingatia matumizi ya kondomu kama kinga ya mambo mawili, kuzuia maambukizi ya VVU na kwa ajili ya kupambana na mimba zisizotarajiwa miongoni mwa wanafunzi wa Chuo Kikuu; ukikolezwa na ujumbe Linda Goli Lako, Kavu Kavu Nomaaa.
Wakati wa Michezo, huduma za upimaji virusi vya ukimwi kwa hiyari na huduma za Afya ya Uzazi kwa ujumla zitatolewa uwanjani hapo bure.

NACP yaja na Mwongozo wa kuhakiki na kuidhinisha matangazo ya VVU na UKIMWI

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI (NACP), mwishoni mwa wiki, ulizindua mwongozo wa Taifa wa Kupitia na Kuhakiki Nyenzo za habari, elimu na mawasiliano ya kubadili tabia kwa lengo la kuboresha habari na mawasiliano yanayofanywa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na wadau wake kwa lengo la kuthibiti kuenea kwa virusi vya UKIMWI (VVU).
Mkuu wa Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano wa NACP Bw. Baraka Mpora akitoa utambulisho wa mwongozo huo kwa wajumbe
NACP iliyopo chini ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ikiwa na jukumu la kusimamia masuala ya kinga, tiba, matunzo na misaada kwenye nyanja ya UKIMWI katika sekta ya afya ncini, imezindua mwongozo huo kwa wadau wa habari, elimu na mawasiliano (IEC) na mawasiliano ya Kubadili Tabia (BCC), mjini Bagamoyo.
Sehemu ya wataalam wa mawasiliano na habari wakisikiliza kwa makini mtoa mada (hayupo pichani) 
Mwongozo huo wa kwanza kwenye sekta ya afya unalenga kuweka viwango vya kitaifa ambavyo wadau wa mawasiliano ambapo nyenzo zote za machapisho na za kielektroniki za IEC/BCC zitapaswa kuhakikiwa na idara hiyo kwa lengo la kuboresha ujumbe inayotolewa.
Lengo kubwa la mwongozo huo ni kuhakikisha matangazo yote yanayohusu kinga, tiba, matunzo na misaada kwenye nyanja ya UKIMWI yanahakikiwa ubora ili kutoa ujumbe sahihi kwa walengwa katika jitihada za serikali za kuunga mkono jitihada za wadau wanaojihusisha na afua za ugonjwa huo nchini.
Dk Mapunda akitoa nasaha wakati wa ufunguzi wa mkutano huo
Katika dibaji ya mwongozo huo, Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Donan Mmbando anasema licha ya juhudi kubwa ya uenezaji na upataji wa shughuli za habari na mawasiliano kuhusu VVU na UKIMWI nchini, bado kuna baadhi ya ujumbe usio sahihi unaotolewa kwa walengwa.
"Ujumbe huo unatofautiana bado ni tatizo kubwa kwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii katika jitihada zake za kutokomeza maambukizo mapya ya VVU pamoja na kutoa matunzo, matibabu na msaada kwa watu wanaoishi na VVU," anasema katika dibaji hiyo na kuongeza;
Majadiliano katika vikundi
"Hali kadhalika usanifu wa viwango visivyofaa vya nyenzo zinazotayarishwa, wakati mwingine hufanya iwe vigumu kwa ujumbe kufikishwa kwa usahihi kwa walengwa waliokusudiwa.
Awali, akimkaribisha mgeni Rasmi katika mkutano huo, kaimu mkuu wa kitengo cha habari elimu na mawasiliano cha NACP, Ndg. Baraka Mpora alisema mwongozo huo umetokana na miongozo ya kitaifa ya kuongeza ubora wa huduma za VVU na UKIMWI iliyotayarishwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kuhakikisha uongezaji ubora wa afua zote kuhusiana na ugonjwa huo unatekelezwa kwa uwiano bora.
Nyenzo zote za machapisho na za elektroniki za IEC/BCC zimekuwa na mikakati mikuu ya inayotumika kuwapasha habari na kuwaelimisha walengwa ili kuinua kiwango cha cha uelewa kuhusu VVU na UKIMWI na kuhimiza makubaliano ya tabia utakaosaidia kupunguza maambukizo mapya ya VVU na maambukizo ya magonjwa ya ngono (STI).
Dk Jesse kutoka Muhimbili akitoa mada kwa washiriki
Wakati wa kuongoza mapitio ya mwongozo huo Afisa Habari na Mawasiliano  wa NACP, Shoko Subira amesema mwongozo huo pia unatoa maelekezo ya usahihi wa matumizi ya nembo inayotumika ikiwa ni pamoja na uwekaji wa nembo ya serikali.
"Kumekuwa na tatizo la jinsi ya kuweka nembo lakini kwa mwongozo huu umeagiza Nembo ya Serikali iwekwe juu ya nembo nyingine au iwe ya kwanza kushoto iwapo nembo zitawekwa kwa ulalo na kufuatiwa na nembo zingine kwa kuwa nembo hii  ni alama ya kitaifa na ni kubwa kwa hadhi kuliko nyingine," akasema Shoko